Monday, July 08, 2013

SHEIKH MKUU WA MISRI ATAKA WAACHIWE HURU VIONGOZI WA IKHWANUL MUSLIMIN

Sheikh Mkuu wa al-Azhar ya Misri, ametoa wito kwa jeshi la nchi hiyo akilitaka liwaachie huru viongozi waandamizi wa Harakati ya Ikhwanul Muslimin ili kupunguza hasira za wafuasi wa Mohammad Mursi, rais aliyepinduliwa wiki iliyopita.
Sheikh Ahmed al Tayyib amesema Misri inaelekea pabaya na ametaka juhudi zifanywe ili kuanza mara moja maridhiano ya kitaifa. Dkt Muhammad Morsi na wenzake wanaendelea kushikiliwa katika kambi ya kijeshi ya Republican Guard mjini Cairo.
Huku hayo yakijiri, Ikhwanul Muslimin imewataka wafuasi wake kupambana na jeshi la nchi hiyo ili kulinda demokrasia. Hii ni baada ya jeshi kuwafyatulia risasi wafuasi wa Dkt. Mursi na kuua zaidi ya 40 kati yao. Jeshi limelazimika kufanya mkutano na waandishi wa habari na kusema wafuasi wa Ikhwani ndio wa kulaumiwa kutokana na mauaji yaliyotokea.
Wakati huohuo nchi mbalimbali zimelitaka jeshi la Misri likomeshe mauaji dhidi ya wafuasi wa Mohammad Morsi. Umoja wa Mataifa pia umeelezea wasiwasi wake kuhusu hali ya mambo nchini Misri. Katibu Mkuu wa UN, Ban Ki-moon amesema hali ya Misri inatia wasiwasi na ametaka hatua za haraka zichukuliwa kulinda maisha ya raia.  

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO