Tuesday, December 04, 2012

THE HAGUE KUSIKILIZA MASHITAKA YA WAPALESTINA

Baada ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kupandisha hadhi ya Palestina katika Umoja wa Mataifa na kuwa nchi mtazamaji asiyekuwa mwanachama rasmi, sasa mahakama ya The Hague huko Uholanzi imetangaza kuwa itaanza kushughulikia mashtaka yaliyowasilishwa na Wapalestina dhidi ya utawala ghasibu wa Israel.

Ofisi ya Mwendesha Mashtaka Mkuu wa mahakama ya The Hague imetangaza kuwa, hivi karibuni itachunguza suala la kupandishwa hadhi ya Palestina katika Umoja wa Mataifa na kushughulikia mashtaka ya Wapalestina kuhusu jinai zilizofanywa na askari wa Israel katika vita vya siku 22 dhidi ya watu wa Gaza.

Mwaka 2009 Wapalestina waliwasilisha mashtaka rasmi katika Mahakama ya Jinai ya Kimataifa ya The Hague wakiitaka ichunguze jinai zilizofanywa na jeshi la Israel katika vita vya siku 22 huko Gaza. Hata hivyo mashtaka hayo yalikataliwa na mahakama ya The Hague kwa kuwa wakati huo Palestina ilikuwa bado haijatambuliwa rasmi kuwa nchi mtazamaji katika Umoja wa Mataifa.

Kwa msingi huo tangu sasa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai itakuwa na uwezo wa kisheria wa kuchunguza na kushughulikia mashtaka yote yanayowasilishwa na Wapalestina. Kwa mujibu wa sheria za kimataifa, nchi ndizo zinazoweza kuwasilisha mashtaka katika Mahakaya ya Kimataifa ya The Hague. Kabla ya uamuzi wa tarehe 29 Novemba wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa ambao uliitambua Palestina kuwa ni nchi mtazamaji, hapakuwepo uwezekano wa kusikilizwa mashtaka ya Wapalestina dhidi ya Israel.

Ni kwa sababu hiyo pia ndio maana utawala ghasibu wa Israel na waitifaki wake wakubwa hususan Marekani wakafanya jitihada kubwa za kukwamisha suala la kutambuliwa Palestina kuwa ni nchi japo isiyo mwanachama katika Umoja wa Mataifa.

Katika mkondo huo huo Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina Mahmoud Abbas alitangaza baada tu ya kurejea Ramallah akitokea New York kwamba, Quds Tukufu ndio mji mkuu wa milele wa nchi ya Palestina. Alisema sasa Wapalestina wamepata nchi na wanaweza kuwasilisha matakwa yao halali katika jamii ya kimataifa. Abbas aliashiria mashinikizo makali yaliyofanyika kwa shabaha ya kuzuia suala la kutambuliwa Palestina kuwa ni nchi mtazamaji katika Umoja wa Mataifa na kusema kuwa, karibu asilimia 75 ya jamii ya kimataifa imewapigia kura ya ndio watu wa Palestina.

Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina amesema kuwa mafanikio hayo yatabadilisha mlingano wa nguvu za kisiasa katika Mashariki ya Kati.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO