Saturday, January 12, 2013

WAZIRI WA KAZI MAREKANI AJUZULU

Zikiwa zimesalia siku 10 tu kabla ya kumalizika kipindi cha kwanza cha utawala wa Rais Barack Obama wa Marekani, Waziri wa Kazi wa nchi hiyo ametangaza kujiuzulu. Hilda Solis Mmarekani mwenye asili ya Uhispania alikuwa Waziri wa Kazi kwa kipindi chote cha karibu miaka minne ya utawala wa Obama. Ijapokuwa Waziri wa Kazi wa Marekani hana majukumu ya kuandaa shughuli za ajira nchini humo, hata hivyo yeye pamoja na White House walikabiliwa na lawama na ukosoaji mkubwa kwa kushindwa kupunguza kiwango cha watu wasiokuwa na ajira nchini humo. Wakati Hilda Solis alipopewa jukumu la kuiongoza wizara hiyo, Wamarekani walitaraji kuona ahadi iliyotolewa na Obama ya kuandaa nafasi milioni mbili na nusu za ajira ikitekelezwa katika kipindi cha miaka mitatu. Licha ya kupita miaka minne nafasi hizo za ajira sio tu hazijapatikana bali idadi ya Wamarekani wasiokuwa na kazi hivi sasa imefikia milioni nne. Hivi sasa kiwango cha watu wasio na ajira nchini Marekani kinakaribia asilimia 7.8 ingawa inatarajiwa kuwa katika miezi ijayo kiwango hicho kitashuka na kufikia asilimia saba. Hata hivyo, duru zisizo rasmi zinaeleza kuwa, kiwango cha ukosefu wa ajira kinafikia mara mbili ya kiwango kilichotangazwa na Wizara ya Kazi ya nchi hiyo. Hilda Solis anahesabiwa kuwa waziri wa tano kujiuzulu tokea Rais Obama alipojipatia ushindi kwenye uchaguzi wa rais uliofanyika Novemba 6, 2012. Kabla ya hapo, Hillary Clinton Waziri  wa Mashauri ya Kigeni, Timothy Geithner Waziri wa Fedha, Leon Edward  Panetta Waziri wa Ulinzi na  Lisa Jackson Waziri wa Hifadhi ya Mazingira  walitangaza kujiuzulu nyadhifa zao. Inatazamiwa kuwa, baraza lijalo la mawaziri la Rais Obama litakuwa na mabadiliko ya mlingano wa kiasili na kijinsia kulinganishwa na baraza la awamu ya kwanza. Hivi sasa, mawaziri watatu wanawake waliokuwa kwenye baraza lililopita yaani Hillary Clinton, Hilda Solis na Lisa Jackson wameshajing'atua na nafasi moja kati ya hizo ya mambo ya nje imeshatangazwa kushikiliwa na mwanamume. Iwapo Maseneta watashirikiana kumpitisha John Kerry kuwa Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje, shakhsia huyo ataliongoza jahazi la wanadiplomasia wa Kimarekani katika kipindi cha miaka minne ijayo. Wamarekani waliokuwa na asili ya Kihispania ambao walikuwa na ushawishi mkubwa katika ushindi wa Obama katika chaguzi za miaka ya 2008 na 2012, hivi sasa wana wasiwasi baada ya kujiuzulu Hilda Solis, kwani umepungua uwezekano wa kupewa tena nafasi za juu kwenye serikali ya Obama. Wakati huohuo Obama amemuarifisha mshirika wake wa zamani katika Baraza la Seneti Chuck Hagel, kuziba nafasi ya Leon Panetta kuiongoza Pentagon. Ijapokuwa Hagen ni seneta aliyebobea kutoka mrengo wa Republican, amma wanachama wenzake wa chama hicho walimtuhumu kwa kuyapuuza maslahi ya utawala wa Kizayuni wa Israel na kwamba hakuonekana kuwa ngangari katika kukabiliana na ushawishi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Kwa minajili hiyo, Lobi zenye nguvu za Kizayuni nchini Marekani ikiwemo Kamati ya Masuala ya Umma ya Marekani na Israel AIPAC iliingilia kati na kuzuia Hagen kuchukua wadhifa nyeti wa kuiongoza Wizara ya Ulinzi. Hali kadhalika, mrengo wa Republican unakosoa John Owen Brennan kupewa jukumu la kuliongoza Shirika la Ujasusi la Marekani CIA. Mrengo huo haukuridhishwa na utendaji wa serikali ya Obama katika kampeni za kupambana na ugaidi akiwemo Brennan mwenyewe ambaye ni mshauri wa rais katika operesheni dhidi ya vitendo vya kigaidi. Mrengo huo unataka Brennan asipewe jukumu la kuiongoza CIA kwa vile alishindwa kuzuia shambulio la Ubalozi wa Marekani huko Benghazi, Libya. Alaa kulli haal, kipindi cha kwanza cha miaka minne cha uongozi wa Obama kimefikia ukingoni ambapo mpasuko wa kisiasa huko Washington umezidi kuwa mkubwa mno katika hali ambayo katika miongo ya hivi karibuni kumeshuhudiwa kila hatua inayochukuliwa na chama kimoja, hukabiliwa na upinzani na radiamali kali kutoka chama kingine.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO