Friday, August 17, 2012

MSIMAMO WA WAISLAMU KUHUSU SENSA 2012


JUMUIYA NA TAASISI ZA KIISLAMU TANZANIA
MSIMAMO WA WAISLAMU KUHUSU SENSA 12

Utangulizi:
Suala la sensa ya watu na makazi ktk Uislamu ni mas’ala yenye mafundisho kutoka kwa Qur’an 8:60 na
kutoka ktk Sunnah ya Mtume (swalla Allwaahu ‘alayhi wasallam) na Makhalifa waongofu.
Katiba ya Jamhuri Ibara ya 18 (1) na (2) inatambua haki ya wananchi kutoa na kupata habari;-
                  “18. -(1) Bila ya kuathiri sheria za nchi, kila mtu yuko huru kuwa na maoni yoyote na kutoa nje
                    mawazo yake, na kutafuta, kupokea na kutoa habari na dhana zozote kupitia chombo chochote
                    bila ya kujali mipaka ya nchi, na pia ana uhuru wa mawasiliano yake kutoingiliwa kati”.
                   “(2) Kila raia anayo haki ya kupewa taarifa wakati wote kuhusu matukio mbalimbali nchini na
                    duniani kote ambayo ni muhimu kwa maisha na shughuli za wananchi, na pia juu ya masuala
                     muhimu kwa jamii”.

Vile vile Umoja wa Mataifa unaelekeza jinsi ukusanyaji wa sensa za watu kwa mujibu wa dini zao
unavyopaswa uwe na kwa kutaja si tu dini za watu bali hata madhehebu zao kama dini ina
madhehebu.

Para 2.109 inasema “For census purposes, religion may be defined as either religious or spiritual belief
of preference, regardless of whether or not this belief is represented by an organized group, or
affiliation with an organized group having specific religious or spiritual tenets”.

Para ya 2.111 inasema “For the benefit of users of the data who may not be familiar with all of the
religions or sects within the country, as well as for purposes of international comparability, the
classifications of the data should show each sect as a subcategory of the religion of which it forms a
part. A brief statement of the tenets of religions or sects that are not likely to be known beyond the
country or region would also be helpful” ( www.unstats.un.org)


2. Historia ya mgogoro wa waislamu kutokushiriki zoezi la sensa 2012
Mgogoro uliopo baina ya serikali na waislamu kuhusu kuwekwa kipengelel cha dini haukuanza ghafla tu. Waislamu wameshiriki sensa zisizo na kipenghelel cha dini pasina malalamiko yoyote tangu ile 1978, 1988 na 2002. Hatukuw ana sababu yoyote kudai kiwekwe kipengele cha dini katika sense pamoja na kutambua kwamba takwimu za mwaka 1967 zilichakachuliwa na pia kuna takwimu feki juu ya idadi ya waislamu na wakristo zipo katika machapisho mbalimbali na mitandao mbalimbali.

Mtazamo wetu ulianza kubadilika tulipoanza kuona kalenda zenye nembo na bendera ya taifa zikiwemo zilizotiolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Takwimu za Bodi ya Utalii, shajara (diary) ya mwaka 2010 iliyotolewa na Wizara ya mambo ya Ndani n.k. zikionesha kwamba idadi ya wakristo nchini ni kubwa kuliko ya waislamu. Takwimu hizi zilimaanisha jambo moja tu- kwamba takwimu hizi zinatambulika kiserikali.

Mgongano wa kwanza kati ya waislamu kwa upande mmoja na serikali na Makanisa kwa upande mwingine kuhusu suala hili la sensa ya mwaka huu ni uliotokea katika mkutano ulioitishwa na idara ya takwimu White Sands Hotel Dar es Salaam ambapo viongozi wa Kikristo na Kiislamu walikutana kujadili maandalizi juu ya sensa.

Waislamu waliitaka idara ya ya takwimu kuthibitisha kama takwimu zilizotolewa na TBC1 siku ya tarehe
26 Aprili, 2012 kwamba wakristo ni wengi kuliko waislamu ambapo wakristo 52% na waislamu 32% na wapagani 16% ni sahihi au la. Mkurugenzi wa Idara ya Takwimu akasema takwimu hizo si sahihi kwa sababu serikali tangu 1967 haijaweka kipengele cha dini katika sensa yoyote ile baada ya hiyo.

Viongozi wa Kiislamu wakaonesha takwimu mbali mbali zilizopo katika maandiko na tovuti mbalimbali na kuitaka idara ya takwimu kwa kuwa inaonekana takwimu hizi za idadi ya wakristo na waislamu zinahitajika nchini na kimataifa, basi katika dodoso la sensa mwaka huu kipengele hicho kiwekwe.

Mkurugenzi wa Idara ya takwimu akasema serikali ilikiondoa kipengele hicho mwaka 1967 kwa ajili ya kuleta umoja wa kitaifa kwa hiyo haiwezi kukiweka. Waislamu walipinga hoja hiyo kwa kusema hakuna ushahidi wowote kwamba umoja wa kitaifa utatoweka kwa kuweka kipengele cha dini na kuna nchi nyingi tu duniani zinatoa takwimu za sensa kwa mujibu wa dini na wala amani haijatoweka.

Mfano Uingereza, India, Kenya, Ethiopia, Uganda, Malawi n.k. Kinachohatarisha amani si kuweka kipengele cha dini katika dodoso la sensa bali hizi takwimu za uongo kwamba watu fulani ni wengi kuliko wengine wakati hakuna sensa iliyofanyika kuhusu suala hili.

Katika mkutano huo wa White Sands, viongozi wa Kikristo wote waliunga mkono kutokuwekwa kipengele cha dini katika sensa. Waislamu walipohoji kama kuna hatari ya kuvunjika umoja wa kitaifa, mbona dodoso la sensa lina kipengele cha makanisa na misikiti? Kama kujua majumba hayo ya ibada hakuvunji umoja wa kitaifa, iweje kujua wafanya ibada au wenye kujinasibisha na majaumba hayo ya ibada kuvunje umoja wa kitaifa? Hakukuwa na majibu bali idara ya takwimu ikashikilia msimamo wake.


Mkutano wa Viongozi wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Dar es Salaam.
Baada ya mkutano wa viongozi wa dini na idara ya takwimu White Sands Hotel, na baada ya kuona msimamo wa serikali ni kutokuweka kipengele che dini, viongozi wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu wakakutana jijini Dar es Salaam tarehe 29 Juni, 2012 kujadili suala hili. Katika mkutano huo, umauzi ulifikiwa kuiandikia idar aya takwimu ombi rasmi la kuitaka iweke kipengele cha dini katika dodoso la sensa la sivyo waislamu hawatoshiriki. Jumuiya na Taasisi ziliandika barua hiyo tarehe 4 Juni, 2012 iliyosainiwa na viongozi wa Mumuiya na Taasisi za Kiislamu isipokuwa Bakwata na zilitoa hadi tarehe 20 Juni, 2012 idara hiyo iwe imefanya hivyo laa sivyo waislamu watasusia zoezi la sensa mwaka huu.

Mkutano wa Dodoma tarehe 11 Juni, 2012
Wakati tukisubiri majibu ya barua yetu kwenda idara ya takwimu, tukapata mwaliko wa idara hiyo tarehe 8 Juni, 2012 kwenda Dodoma kuhudhuria semina ya siku moja ya viongozi wa dini juu ya masuala ya sensa .

Katika semina hiyo, waislamu wakalileta tena suala hili mbele ya idara ya takwimu na likajadiliwa na pande tatu – wakristo, waislamu na serikali. Msimamo wa viongozi wa kikristo na serikali ukawa kama siku ya mkutano wa White Sands Hotel kwamba serikali haitoweka kipengele cha dini. Baada ya waislamu kutoa hoja zisizojibika, TBC1 ikalazimika kukanusha tena takwimu walizozitoa kama moja ya juhudi za kuwafanya waislamu waache msimamo wao.

Hatimaye viongozi wa idara ya takwimu wakakubali kuchukua maoni ya waislamu na kuahidi kuyafanyia kazi. Lakini wakati akifunga semina hiyo, Waziri Ofisi ya Rais Sera na Uhusiano Mhe.Stephen Wasira, alitoa msimamo wa serikali kwamba “serikali haiwezi kuweka kipengele cha dini kwa sababu haipangi maendeleo kwa kipengele cha dini!!!Huku waislamu wakijua kuwepo kwa MoU kati ya Makanisa na Serikali, serikali kupanga mipango ya maeneo ya ibada, makaburi n.k. kwa dini mbali mbali” Waislamu walipotaka kuhoji, waziri alikataa na kuwaambia “kama ninyi hamkuelewa somo wenzenu (wakristo) wameelewa”, kauli ya kejeli kwa masheikh na viongozi wa Kiislamu waliohudhuria pale.

Viongozi wa Kiisalamu waliohudhuria semina hiyo jioni ya siku hiyo wakakaa na kuandika barua ya pamoja kwa idara ya takwimu kupinga msimamo huo wa serikali na kauli za kejeli za Mhe. Wasira kwa viongozi wa Kiislamu. Barua hiyo ikasainiwa na viongozi wote wa wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu waliohudhuria semina hiyo ambao wanafikia 31 wakiwemo Bakwata.

Mkutano wa pili wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Dar es Salaam 13 Juni, 2012
Baada kurejea Dar es Salaam, masheikh na viongozi wa Jumuiya na Taasisi mbali mbali za Kiislamu walipokea taarifa ya wajumbe waliokwenda Dodoma na kuijadili ambapo paliamuliwa itolewe Press Release kwa vyomboo vya habari kusisitiza msimamo wa kutokushiriki sensa kwa kuwa serikali imepuuza madai ya waislamu pasina hoja za msingi.

Press Conference ikafanyika Makao makuu ya Bakwata Kinondoni na likatoka tamko rasmi la waislamu
kwamba hawatoshiriki sensa ya mwaka 2012 hadi yafuatayo yafanyike;-
                 1. Kipengelel cha dini kiwekwe katika dodoso la sensa.
                 2. Kuwepo na uangalizi wa pamoja kati ya waislamu na wakristo kwa kuwa tayari kila upande
                  unadai wao ni wengi kuliko upende mwingine.


Tamko la Mufti wa Bakwata kuwataka waislamu kushiriki sensa.
Katika hali iliyotarajiwa na wengi na isiyo ya kushangaza, Mufti wa Bakwata akaitisha mkutano na waandishi wa habari Makao Makuu ya Bakwata tarehe 24 Juni, 2012 na kuwataka waislamu kushiriki sensa kwa sababu haina tatizo.

Viongozi wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu wakalipokea tamko hili na kulipuuza kwa sababu tangu mwanzo Mufti wa Bakwata alitangaza kuunga mkono tu msimamo wa Jumuiya na Taasisi za Kiisalmu akiwa Tanga kwa hiyo maamuzi hayo ni maamuzi yake binafsi au san asana ni ya Bakwata tu. Jumuiya na Taasisi zikaamua kuendelea na msimamo wa awali wa kutokushiriki sensa na msimamo huu ukatolewa tarehe 27 Juni, 2012 mbele ya waandishi wa habari lamada Hotel Dar es Salaam.

Na huu ndio msimamo wa Jumuiya na Taasisi hadi hapo serikali iamue kutekeleza matakwa hayo mawili kabla ya muda wa sensa ijayo kuanza kwa mwezi mzima ili kuruhusu Jumuiya na Taasisi kutoa tena maelekezo kwa waumini wake kushiriki sensa. Kama hili halikufanyika ni wazi kwamba tutakuwa khiyari ila kutekeleza maamuzi ya viongozi wa Jumuiya na Taasisi.


3. Historia ya Sensa Tanzania
Sensa imefanyika hapa nchini mara nane tangu ukoloni- 1921, 1931, 1948, 1957, 1967, 1988, 1978, 2002 na inatarajiwa kufanyika tena mwaka huu 2012. Lengo la sensa ya watu na makazi ni kuiwezesha serikali na wananchi kujua idadi ya watu na hali za makazi yao na hivyo kusaidia mipango ya maendeleo ya serikali nay a jamii husika na hat akuwawezesha wayu kudai haki zao.

Ingawa jamii mbali mbali zinaweza kujihesabu zenyewe, bado sensa inayoendeshwa na serikali ndiyo inayotambulika kisheria kitaifa (credibile) na kimataifa. Ndiyo maana idara ya takwimu ya taifa ilikanusha takwimu hizo baada ya kutakwa na waislamu kutoa kauli juu ya takwimu mbali mbali za idadi ya waislamu na wakristo, ikiwemo ile iliyotolewa na TBC1 siku ya Muungano mwaka huu.

Sensa ya mwisho kuwa na kipengele cha dini ni ile ya mwaka 1967 ambayo kwa mujibu wa wanahistoria ilichakachuliwa kwa maslahi ya kisiasa kuonesha wakristo ni wengi kuliko waislamu (Wapagani 34.3%, Wakristo 33.5% na Waislamu 31.4%). Katika kitabu Globalization, modernization, and education in Muslim countries mwandishi Rukhsana Zia ameandika;-
           “However, according to the first post-independence census of 1967, Christians were 32 percent,  
            Muslims 30 percent ... Unfortunately, that controversial 1967 population census was the last one to
            show religious distribution in Tanzania”.

Kwa hiyo sensa ya mwaka 1967 ilikuwa na kipengele cha dini lakini takwimu, zake ambazo ndizo zilizoweka msingi wa takwimu za sasa zinazoonesha wakristo kuwa wengi kuliko waislamu, zilichakachuliwa kwa makusudi ili kuonesha kuwa wakristo ni wengi kuliko waislamu kuhalalisha dhulma mbali mbali ambazo waislamu wamekuwa wakifanyiwa katika elimu, madaraka, ajira, uchumi na huduma za jamii.

Madai ya waislamu kuwa pawekwe kipengele cha dini katika sensa hii ni juhudi za kudai haki na uadilifu utendeke kuhusu takwimu za idadi ya waislamu na wakristo nchini ili takwimu zisipotoshwe tena. Kwa hiyo msimamo wetu si wa kubahatisha hata kidogo, ni msimamo wa haki na unastahiki kuungwa mkono na wapenda haki wote.


5. Faida za kujua idadi ya wananchi kwa mujibu wa dini zao.
Faida ziko nyingi kwa sababu matumizi ya takwimu za idadi ya watu kwa mujibu wa dini zao ni mengi.
        i) Zitawezesha kuondoa utata uliopo na kujua takwimu za kweli. Taifa halipaswi kutegemea takwimu za
           uongo kuhusu idadi ya rai wake kwa mujibu wa dini zao.
       ii) Takwimu sahihi za watanzania kwa mujibu wa dini zao zitaiwezesha serikali makini kujua mahitajio
           halisi ya wana dini ingawa serikali haina dini. Katiba kusema serikali haina dini haina maana kwamba
           ndiyo isijishughulishe na mahitaji ya kidini ya raia wake. Ndiyo maana serikali imetoa misamaha ya
           kodi kwa mashirika ya dini ili yaweze kuhudumia wana dini wao.
      iii) Serikali hutenga maeneo mbali mbali kwa ajili ya majumba ya ibada na shughuli nyingine za kidini
           kama vile makaburi. Kwa kujua takwimu hizi, serikali itapanga vizuri mipango hiyo kwani itakuwa
           inazo takwimu halisi za idadi ya watu wake kwa mujibu ya dini zao. Kama serikali isipojua idaidi ya
           wafuasi wa dini fulani itawezaje kugawa maeneo hayo sawasawa kwa mujibu wa idadi ya wana dini
           mbali mbali? Ndiyo maana kwa kutumia takwimu feki zilizoko serikali hugawa maeneo makubwa
           makubwa kwa wakristo na waislamu kuambulia maeneo madogo tu.
      iv) Serikali mara nyingi inahimiza viongozi wa dini kuwaelimisha waumini wao juu ya masuala mbali mbali  
           kama vile uharibifu wa maadili, Ukimwi na VVU, madawa ya kulevya, ulinzi shirikishi n.k. Kama
           serikali itajua idaidi ya watanzania kwa dini zao itaweza kuelewa wka uhakika ni watu wangapi
           wanafikiwa na mipango ya serikali kupitia dini zao.

       v) Wawekezaji na wagenii mbali mbali wakiwemo watalii wanaotembelea Tanzania, kwa mujibu wa
           utaratibu wa kimataifa, hutaka kujua habari mbali mbali juu ya nchi yetu ikiwemo takwimu ya idadi ya
           watu, makabila yao, dini zao n.k. ili wajiandae kukabiliana na mazingira yetu ya kimaadili na
           kiutamaduni. Kujua takwimu rasmi zilizotolewa na serikali kutawasaidia wawekezaji na hata watalii
           kuwajua watanzania kwa mujibu wa dini zao.

     vi) Hali kadhalika, wana dini husika, ingawa kila dini inao utaratibuwa kujua wafuasi wake, watanufaika
          na takwimu za idadi ya watu kwa mujibu wa dini zao kwani takwimu zitakazotolea kwa mujibu wa
          sensa ya serikali zinapatikana kwa upana zaidi (comprehensive) kuliko zile zinazokusanywa na dini
          husika. Kwa hiyo zitasaidia hata viongozi wa dini kupanga mipango yao ya kuwahubiria watanzania
          maadili mema, kupinga maovu na uhalifu na hivyoo kuchangia amani iliyopo.


5. Kama Serikali haitoweka kipengele cha dini katika dodoso la sensa msimamo wetu ni nini?
Katika mazingira yaliyopo ambapo dodoso la sensa limeweka kipengele cha majumba ya ibada (kanisa alama ya Msalaba, msikiti alalama ya mwezi mchanga na nyota) na hata makaburi, ambayo kwa bahati mbaya alama yake ni misalaba mitatu (pengine kuwakilisha TEC, CCT na PCT) hakuna alama ya makaburi ya waislamu, tunahisi kwamba zoezi zima hili linafanyika kwa maslahi ya Kanisa.

Kwa mujibu wa hali tunayoiona na kwa mujibu wa takwimu zinazoonesha kwamba wakristo nchini ni wengi kuliko waislamu ambazo tayari zinatolewa na Makanisa na hata idara za serikali na mashirika ya nje ya nchi, tunaona kwamba kushiriki kwetu katika sensa hii kabla ya kipengele cha dini kuwekwa na kabla ya kuhakikisha kwamba mazingira ya kuchakachuliwa takwimu kama ilivyotokea 1967 hayajawekwa ni sawa na kujitia kitanzi wenyewe kwa kuhalalisha dhulma dhidi ya waislamu.

Iwapo serikali itaweka kipengele cha dini katika sensa na kuweka mazingira ya uangalizi wa pamoja wa waislamu na wakristo (observers) hata pasina kugharimiwa na serikali kufuatilia zoezi la sense kuanzia kuhesabu, kujumlisha na kutoa matokeo angalau mwezi mmoja kabla ya zoezi hili, tutaangalia uwezekano wa kushiriki katika zoezi la sensa mwaka huu.

6. Kuhusu zoezi la Vitambulisho vya Taifa
Jumuiya na Taasisi hazina kipingamizi chochote juu ya zoezi hili ingawa hadi sasa hatuna maelezo yoyote ya kina juu yake na tunachunguza mwenendo mzima kisha tutawaambia waislamu.Iwapo pia tutagundua udini katika zoezi hili, hatutasita kuwaambia waislamu juu ya dosari zilizopo. Hata hivyo hadi sasa kuna kipengele kilichoandikwa “Cheti cha Ubatizo/Falak…….” ambacho kwa kuwa kuna mialiko imetoka kuwaita masheikh na maimamu kwenye semina juu ya zoezi la vitambulisho vya taifa, tutaulizia huko.

Hali kadhalikak wasi wasi wetu ni kwamba huonda zoezi hili likatumika kuongeza idadi ya wakristo kwa sababu kielelezo kimojawapo kinachotumika ni cheti cha ubatizo wakati katika waislamu hakuna cheti ya utambulisho bali Shahada “Laa ilaaha illa-llwaahu Muhammadan Rasuulu-llwaahu” tu. Wenye vyeti ni wale waliosilimu tu.

Wabillahi Tawfiiq

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO