Thursday, March 28, 2013

WAPIGAMBIZI WATATU WAKAMATWA WAKIKATA MKONGA WA INTERNET ULIO CHINI YA BAHARI


Maafisa wa utawala nchini Misri, wamewakamata wapigambizi watatu waliokuwa wanajaribu kuukata mkonga wa internet ulio chini ya bahari. Wanaume hao walikamatwa wakiwa katika boti walilokuwa wanatumia kwa shughuli za uvuvi, katika mji wa bandarini wa Alexandria. Hii ni kwa mujibu wa msemaji wa jeshi kanali, Ahmed Mohammed Ali. Mkonga huo ulioharibiwa, ulizuia kasi ya huduma za internet nchini Misri na katika nchi nyingine.
Hata hivyo haikubainika ikiwa kupungua kwa kasi ya internet ilihusika moja kwa moja na kitendo cha watatu hao kuuharibi mkonga ijumaa iliyopita. Wakati huo, kampuni inayomiliki mkonga huo, Seacom, ilisema kuwa mitandao kadhaa iliyounganisha Ulaya na Afrika , Mashariki ya kati na Asia ya Mashariki, iliathirika na hivyo kupunguza kasi ya huduma za internet. Mkonga uliovamiwa Jumatano ulikuwa ule uliounganisha huduma za internet katika nchi za Asia mashariki na Ulaya Magharibi.
Uvamizi ulitokea umbali wa mita 750 Kaskazini mwa Alexandria. Katika taarifa kwenye ukurasa wake wa Facebook Kanali Ali, alisema kuwa wapiga mbizi hao walikamatwa wakati wakivamia mkonga wa kampuni rasmi ya mawasiliano nchini Misri. Hata hivyo hakutoa maelezo yoyote kuhusu nia ya wapiga mbizi hao.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO