Saturday, January 19, 2013

MAREKANI YAITAMBUA RASMISERIKALI YA SOMALIA


Hillary Clinton Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Marekani amesema kuwa, serikali ya Washington inaitambua rasmi serikali ya Somalia. Clinton ameyasema hayo akiwa pamoja na Rais Hassan Sheikh Mahmoud wa Somalia mbele ya waandishi wa habari mjini Washington. Sheikh Mahmoud alijipatia ushindi kwenye uchaguzi mkuu uliofanyika mwaka 2012, na kupata fursa ya kuiongoza nchi hiyo iliyokumbwa na machafuko. Somalia iliyoko katika eneo la Pembe ya Afrika inahesabiwa kuwa nchi iliyoko katika eneo nyeti na la  kiistratijia. Nchi hiyo ilianza kutumbukia kwenye machafuko na mapigano ya wenyewe kwa wenyewe baada ya kuanguka utawala wa Jenerali Muhammad Siad Barre, dikteta wa zamani wa Somalia mwaka 1991. Miaka miwili baada ya kuangushwa utawala wa Jenerali Siad Barre, uhusiano wa Marekani na Somalia ulivunjika baada ya helkopta mbili za Marekani kuangushwa nchini humo. Kundi la al Shabab liliweza kudhibiti eneo kubwa la nchi hiyo wakati wa kukosekana serikali kuu nchini. Amma mwaka 2011, kundi la al Shabab lilipoteza udhibiti wake katika maeneo mengi nchini humo, baada ya kukabiliwa na mashambulio makali ya majeshi ya serikali ya Somalia yakishirikiana na  vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Afrika. Kulegalega na kurejea nyuma kundi la al Shabab kuliandaa mazingira ya kupatikana uthabiti kwa kiasi fulani, kuundwa katiba mpya, kuitishwa uchaguzi huru wa rais na hatimaye kuteuliwa Waziri Mkuu aliyeunda serikali mpya nchini humo. Serikali ya Somalia iliyoingia madarakani mwaka 2012, ilipongezwa na kukaribishwa na jamii ya kimataifa. Hali ya machafuko na ukosefu wa amani nchini Somalia na eneo zima la Pembe ya Afrika iliwatia hofu Wamarekani na waitifaki wake wa eneo la Mashariki ya Kati na utawala wa Kizayuni wa Israel. Hakuna shaka kuwa, meli za kibiashara na kijeshi za Israel zilikuwa na wasiwasi kupita katika eneo la lango la Bab Mandab lililoko katika eneo la Pembe ya Afrika. Ukosefu wa amani nchini Somalia, uliligeuza eneo hilo kuwa mgogoro wa kimataifa baada ya kujitokeza vitendo vya uharamia nchini humo. Kwenye mazungumzo na Rais Sheikh Mahmoud wa Somalia, Clinton amesema kuwa, Washington na Mogadishu zimefungua ukurasa mpya wa uhusiano wao na kusisitiza kuwa, Washington itakuwa mshirika kindakindaki wa Mogadishu. Naye Rais Barack Obama wa Marekani ameahidi kuwa nchi yake itashirikiana na Somalia katika kunyanyua kiwango cha usalama na amani, utunzaji wa fedha na kuandaa mazingira ya kutolewa huduma za kijamii nchini humo. Mashirikiano ya pande mbili yataweza kufanikiwa kwanza kwa kutambuliwa rasmi nchi hiyo, jambo ambalo tayari limeshatamkwa wazi na Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Marekani mbele ya Rais wa Somalia mjini Washington.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO