Saturday, January 12, 2013

MWITO WA KURA YA MAONI KUHUSU UFALME WA UINGEREZA


Mbunge mmoja nchini Uingereza amekosoa vikali kukosekana demokrasia nchini humo akihoji kwa kusema kwa nini wananchi wa nchi hiyo hawana haki ya kutoa maoni yao kuhusu mtu wa kurithi kiti cha Malkia Elizabeth na ametaka kufanyike kura ya maoni kuhusu suala hilo. Paul Flynn kutoka chama cha Leba amesisitiza kuwa, ni jambo la dharura kuitishwa kura ya maoni ya kuamua iwapo mkuu wa serikali ya Uingereza yaani Waziri Mkuu, ambaye anachaguliwa na wananchi, anawajibika kumfuata Malkia au la, pamoja na kufanyia marekebisho sheria za mrithi wa Malkia wa ufalme wa Uingereza. Kwa mujibu wa Katiba iliyodumu kwa muda mrefu nchini Uingereza ni kuwa, Malkia ni cheo cha juu zaidi rasmi nchini humo licha ya kwamba hachaguliwi kidemokrasia na ana majukumu mengi ya kidiplomasia na ya rasmi kama vile kuidhinisha Waziri Mkuu. Malkia wa Uingereza aidha ndiye Amirijeshi Mkuu wa vikosi vyote vya Ulinzi vya nchi hiyo licha ya kwamba wananchi hawana nafasi yoyote ya kutoa maoni yao kuhusu nani awe Malkia na nani arithi kiti chake. Kumekuwa na malalamiko mengi ndani ya Uingereza kuhusu ufujaji mkubwa wa mali unaofanywa na familia ya kifalme ya nchi hiyo. Malalamiko hayo yaliongezeka sana baada ya mwana mfalme William kufanya sherehe ya harusi iliyojaa ufakhari na anasa kubwa kwa kufuja fedha za walipa kodi wa Uingereza. Mirengo inayopinga kuendelea mfumo wa kifalme nchini Uingereza imeitisha maandamano ya wananchi wakati wa sherehe za miaka 60 ya utawala wa mfululizo wa Malkia wa hivi sasa wa Uingereza. Mirengo hiyo inataka wananchi wa Uingereza wawe na nguvu ya mwisho wa kuamua watawaliwe na nani na kwa msingi wa katiba gani. Naye Graham-Smith, mkurugenzi mtendaji wa taasisi ya kiraia inayopinga mfumo wa kifalme nchini Uingereza inayojulikana kwa jina la "Jamhuri" amesema kuwa, tofauti na propaganda kubwa zinazofanywa na vyombo vya habari vya Uingereza ambavyo kisingi vinadhibitiwa na familia ya kifalme, wananchi walio wengi wa Uingereza hawapendi kuendelea kutawaliwa na mfumo ambao hauwapi haki ya kuchagua viongozi wake. Naye Dk. Adrian Thurston, mkuu wa jumuiya ya wasomi ya "Lyceum" ya mjini London amelalamikia vikali jinsi serikali ya Uingeza inavyofuja mamilioni ya fedha za umma kwa ajili ya kudhamini maisha ya anasa na yaliyojaa starehe ya watu wa familia ya kifalme. Hata hivyo vyombo vya habari vya Uingereza vinajaribu kuficha kikamilifu mitazamo ya wananchi wa nchi hiyo kuhusu Malkia na mara zote vinaonesha kuwa wananchi wa Uingereza wanampenda kupindukia Malkia wa nchi hiyo. Hata hivyo weledi wa mambo wanaamini kuwa si jambo rahisi hata kidogo kukubaliwa pendekezo la kuitishwa kura ya maoni huko Uingereza kwani viongozi walioko madarakani wanajua vyema kuwa iwapo kura hiyo ya maoni itaitishwa, basi wananchi wataukataa bila kusita mfumo wa kifalme ambao hauwapi haki ya kuchagua. Aidha weledi hao wa mambo wanahoji wakisema, vipi nchi kama Uingereza inazishinikiza nchi nyingine bali hata kuzivamia kijeshi baadhi ya nchi hizo kwa madai ya kueneza demokrasia wakati Malkia wa Uingereza yuko madarakani kwa zaidi ya nusu karne sasa tena bila ya kuchaguliwa hata kwa kura moja ya wananchi

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO