Saturday, January 12, 2013

SHEIKH MKUU WA BAHRAIN ATAKA WANANCHI KUSIKILIZWA

Sheikh Issa Qassim Mkuu wa Baraza la Wanazuoni nchini Bahrain amesema kuwa, njia pekee ya kuutokomeza  mgogoro wa nchi hiyo, ni kuheshimiwa  irada za wananchi wa Bahrain. Akihutubia mjumuiko mkubwa wa waumini kwenye ibada ya Ijumaa  huko Manama, mji mkuu wa Bahrain Sheikh Issa Qassim amesisitiza kuwa irada ya wananchi wa nchi hiyo ni kutekelezwa matakwa yao na kuongeza kuwa, njia pekee ya kuukwamua mgogoro wa Bahrain ni kutambuliwa rasmi matakwa ya wananchi na kutekelezwa kwa mujibu wa sheria. Sheikh Qassim amesema kuwa, kuna udharura kwa utawala wa Aal Khalifa nchini humo kuangalia upya siasa zake za ukandamizaji dhidi ya wananchi na kusisitiza kuwa, utawala huo unapaswa kuwaachilia huru shakhsia, wanasiasa na wanaharakati wengine wa kutetea haki za binadamu ambao hivi sasa wanashikiliwa magerezani kwa makosa ya kupigania haki zao. Mahakama ya Rufaa ya Bahrain siku ya Jumatatu iliyopita ilithibitisha hukumu iliyotolewa dhidi ya wanaharakati 13 wa kisiasa nchini humo, ambapo saba kati yao walihukumiwa kifungo cha maisha jela, wanne kifungo cha miaka 15 na wawili walihukumiwa kifungo cha miaka mitano jela.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO