Friday, April 26, 2013

DRONE NYINGINE YA HIZBULLAH YATUNGULIWA ISRAEL

Jeshi la utawala haramu wa Kizayuni limetangaza kutungua ndege isiyo na rubani (dron) inayodaiwa kumilikiwa na Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Hizbullah ya Lebanon karibu na bandari ya kaskazini mwa Haifa huko katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu. Shirika la Habari la AP limemnukuu Msemaji wa Jeshi la utawala huo haramu akisema kuwa, ndege hiyo ilitambuliwa ikiwa katika anga ya Lebanon katika umbali wa kilometa nane kutoka pwani ya magharibi mwa Haifa na kudondoshwa na jeshi la Israel. Kwa mujibu wa shirika hilo, ndege iliyokuwa imembeba Waziri Mkuu wa utawala haramu wa Kizayuni, Benjamin Netanyahu ambaye alikuwa katika ziara ya kutembelea eneo la kaskazini mwa ardhi hizo za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu, ililazimika kutua kwa dharura kufuatia ndege hiyo isiyo na rubani kuingia katika anga ya Israel. Aidha Netanyahu amenukuliwa akisema kuwa, tukio hilo ni zito mno. Hadi sasa meli za utawala huo zinaendelea kutafuta mahali ndege hiyo ilipodondokea. Itakumbukwa kuwa mnamo mwezi Oktoba mwaka jana Israel ilitungua ndege nyengine isiyo na rubani ya harakati hiyo ya Hizbullah suala lililoipelekea Israel kushikwa na wasi wasi mkubwa hadi leo.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO