Saturday, April 27, 2013

HALI YA HATARI KATI YA ISRAEL NA LEBANON


Jeshi la Lebanon limejiweka tayari kuanzia asubuhi ya leo kufuatia madai yaliyotolewa na utawala haramu wa Israel ya kudungua ndege isiyo na rubani katika anga ya mji wa Haifa inayodaiwa kumilikiwa na harakati ya Hizbullah.
Chanzo kimoja cha usalama katika jeshi la Lebanon kimesema kuwa, majeshi ya Lebanon yaliyoko katika mipaka ya ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na utawala huo bandia yamewekwa katika hali ya tahadhari kubwa. Chanzo hicho pia kimesisitiza kuwa, jeshi la Israel limeongeza idadi ya askari wake hususan katika maeneo ya mashariki ya Mazariu Shaba'a na karibu na lango la Fatwimah huko Kufru Kalaa na eneo la Ghajar na kando na eneo la Abbasiyyah nchini Lebanon. Jeshi la utawala wa Kizayuni pia limeweka vifaru vya kivita aina ya Merkava katika maeneo kadhaa ya mpakani sambamba na kurusha idadi kadhaa ya ndege zake zizizo na rubani katika maeneo hayo.
Hapo jana jeshi la utawala haramu wa Israel lilitangaza kuwa, lilitungua ndege isiyo na rubani inayodaiwa kumilikiwa na harakati ya Hizbullah ya Lebanon karibu na bandari ya kaskazini mwa Haifa katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu.
Hizbullah ya Lebanon imekanusha madai kuwa ilituma ndege isiyokuwa na rubani (drone) katika ardhi zinazokaliwa kwa mabavu za Palestina huko Israel.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO