Saturday, April 20, 2013

MATATIZO MAKUBWA YAZIDI KUUKUMBA UKANDA WA GHAZA


Kamati ya Wananchi ya Kupambana na Mzingiro katika Ukanda wa Gaza imetangaza kwamba wakazi wa ukanda huo wanakabiliwa na mgogoro mkubwa wa uhaba wa umeme, maji safi ya kunywa na matatizo ya kiafya. Utawala haramu wa Israel umekuwa ukiuzingira ukanda huo tokea angani ardhini na baharini tangu mwaka 2006, jambo ambalo limewasababishia wakazi wake matatizo mengi ya kiuchumi, kiafya na kijamii. Suala hilo limezipelekea taasisi muhimu za kimataifa ukiwemo Umoja wa Mataifa, mashirika ya haki za binadamu, wataalamu na shakhsia mbalimbali wa kieneo na kimataifa kuonya kwamba mgogoro na maafa ya binadamu yanaweza kutokea wakati wowote katika ukanda huo. Tatizo kubwa zaidi kati ya matatizo hayo ni uhaba na kukatwa mara kwa mara umeme na utawala haramu wa Israel, jambo ambalo limewaletea machungu mengi wakaazi wa ukanda huo.
Hatua ya utawala haramu wa Tel Aviv ya kukata umeme mara kwa mara katika misimu ya vipindi baridi imewalazimu wakazi wa Ukanda wa Gaza kutumia mishumaa kuleta joto katika nyumba zao suala ambalo mara nyigi limekuwa na matokeo hatari ya kuteketea kwa nyumba hizo na kuwaua wanaoishi humo. Hivi sasa ambapo kipindi cha joto kinakaribia ukataji huo wa umeme unaweza pia kuwa na matokeo mabaya kwa wakazi wa Ukanda huo. Uhaba wa maji safi pia umekuwa na madhara makubwa kwa wakazi wa Gaza wapatao milioni 1.7. Licha ya hayo maji yanayoruhusiwa kuingia katika Ukanda wa Gaza na utawala haramu wa Israel hayaoani na viwango vya kimataifa vilivyoainishwa na Shirika la Afya Duniani WHO. Asilimia 95 ya maji yanayotumiwa na wananchi wa Gaza ni ya chumvi na asilimia 5 iliyosalia pia imechanganyika na mada za kemikali ambazo humwagwa kwenye maji hayo na utawala wa Israel. Sehemu kubwa ya wananchi hao pia hawana uwezo wa kiuchumi wa kijidhaminia maji hayo ambayo huuzwa kwa bei ghali na wafanyabiashara wa Kizayuni. Sababu kuu ya kuenea magonjwa mbalimbali katika Ukanda wa Gaza ni kiwango cha chini cha maji wanayokunywa na kutumia katika kukidhi mahitaji yao mengine. Ni kutokana na ukweli huo ndipo Shirika la Afya Duniani likaonya mara kwa mara katika ripoti zake kuhusiana na hatari ya kiafya katika Ukanda wa Gaza. Hii ni katika hali ambayo utawala wa Israel unatumia maji safi yanayopatikana katika Ukanda wa Gaza katika kunyunyizia ardhi zake za kilimo.
Uhaba wa madawa na mahitaji ya kiafya ni tatizo jingine muhimu linalowasumbua wakazi wa Ukanda wa Gaza, tatizo ambalo likichanganyika na matatizo mengine tuliyoyazungumzia mwanzoni linaweza kusababisha mkasa  mkubwa wa kibinadamu katika Ukanda wa Gaza. Hii ni katika hali ambayo idadi ya wagonjwa wanaotatizwa na magonjwa mbalimbali katika ukanda huo imeongezeka sana katika siku za hivi karibuni. Awali shirika la WHO lilitahadharisha kwamba litalazimika kufunga idadi kadhaa ya vituo vyake vya afya katika Ukanda wa Gaza kutokana na kutokuwa na madawa pamoja na vifya vya kutosha vya matibabu. Kutokana uhaba huo idadi kubwa ya wagonjwa wa Gaza tayari wapekwishapoteza maisha yao na wengine wanasubiri tu mauti katika nyumba zao au katika vituo vya afya visivyokuwa na vifaa vyovyote vya kuwatibu.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO