Saturday, August 17, 2013

VIKOSI VYA USALAMA MISRI VYAUZINGIRA MSIKITI

Vikosi vya usalama nchini Misri, vimeuzingira msikiti uliojaa wafuasi wa rais aliepinduliwa Mohammad Mursi mjini Cairo, huku waandamanaji wakipanga maandamano mengine hii leo, baada ya mapigano ya mitaani hapo jana kusababisha vifo vya zaidi ya watu 80.
Kuzingirwa kwa msikiti wa Al-Fatih kumefuatia mapigano makali yaliyosababisha kuuawa kwa watu 83 nchini kote, na kukamatwa kwa wafuasi wengine zaidi ya 1000 wa Rais aliyepinduliwa Muhammad Mursi. Mwandamanaji moja alisema zaidi ya watu 1000 wamekwama katika msikiti huo. Ukandamizaji wa vyombo vya usalama umeigawa Misri zaidi, na kulaaniwa na jamii ya kimataifa.
Ujerumani ilitangaza kusitisha msaada wake kwa Misri, na Kansela Angela Merkel na rais Francois Hollande wa Ufaransa walipendekeza uitishwe mkutano wa dharura wa mawaziri wa mambo ya kigeni wa Umoja wa Ulaya, ili kuwe na msimamo wa pamoja kuhusiana na hali inayoendelea Misri.
Mkuu wa sera za kigeni wa Umoja wa Ulaya Catherine Ashton alisema jana kuwa idadi ya vifo katika siku chache zilizopita inashtua, na kwamba serikali ya muda na uongozi mzima wa kisiasa nchini Misri, wanawajibika kutokana na vifo hivyo.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO