Wednesday, December 12, 2012

UTAWALA WA KIZAYUNI: MADAKTARI WAENDELEA NA MGOMO

             Wafanyakazi wa vituo vya afya katika utawala wa Kizayuni wa Israel wameendelea na mgomo wao kufuatia hatua ya utawala huo ya kupuuza matakwa yao. Wafanyakazi hao wa vituo vya afya na wauguzi katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu, walifanya mgomo hapo siku ya Jumatatu kwa siku ya nane mfululizo katika kulalamikia hatua ya utawala huo ya kutowaongezea mishahara sambamba na kufumbia macho hali yao mbaya ya kimaisha. Aidha wafanyakazi hao wamesistiza kuwa, mgomo huo utaendelea. 


Wauguzi pia wamesema kuwa, pamoja na maafikiano yaliyofikiwa kati yao na Wizara ya Fedha ya Utawala haramu wa Kizayuni katika kipindi cha miezi kadhaa iliyopita, kuhusiana na nyongeza ya mishahara na kuboreshwa kwa mazingira ya kazi, wizara hiyo haikutekeleza ahadi zake hatua iliyowafanya waendelee na mgomo. Kwa mujibu wa ripoti hiyo, mgomo huo umeathiri pakubwa shughuli za baadhi ya mahospitali na vituo vya afya vya utawala wa Israel. 


Mgomo huo wa wafanyakazi wa vituo vya afya na wauguzi unaendelea katika hali ambayo, Wizara ya Fedha ya utawala huo ilikuwa imetishia kuwa, kama mazungumzo kati yake na Muungano wa Wauguzi hayatafikia mwafaka na wauguzi kuendelea kugoma, itawasilisha kadhia hiyo mahakamani kwa ajili ya kuwarejesha kazini kwa nguvu wauguzi wanaogoma. Duru mpya ya mazungumzo kati ya Wizara ya Fedha ya Utawala Haramu wa Kizayuni na Muungano wa Vyama vya Wauguzi, unatazamiwa kufanyika leo Jumatano. 

Ikiwa ni katika juhudi za kupunguza nakisi ya bajeti na kuokoa uchumi unaoelekea kuporomoka wa utawala wa Israel, Baraza la Mawaziri chini ya uongozi wa Benjamin Netanyahu Waziri Mkuu wa utawala huo, limeanza kutekeleza siasa za kubana matumizi jambo ambalo limekabiliwa na upinzani mkali wa raia wa utawala huo. 


Katika hali hiyo, Mkuu wa Muungano wa Wauguzi wa Israel amenukuliwa akisema kuwa, sekta ya uuguzi ya utawala huo inakabiliwa na mgogoro mkubwa kufuatia idadi kubwa ya wauguzi kupungua katika miaka ya hivi karibuni na hivyo kuathiri shughuli za afya katika mahospitali mbalimbali. Hivi sasa vituo vya afya vya Tel Aviv, vinakabiliwa na upungufu wa wauguzi wapatao 2400, ambapo wauguzi 400 huongezeka kila mwaka katika idadi hiyo. Matatizo ya kiuchumi na migomo mbalimbali katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu, inajiri wakati ambao polisi ya Israel imetoa ripoti rasmi kuhusiana na ongezeko la uhalifu na jinai katika utawala huo. Ufisadi wa kimaadili, kifedha na kiidara kati ya watawala wa kijeshi na kisiasa wa Israel, ni matatizo mengine yanayoukabili utawala huo, jambo ambalo limepelekea kuzuka upinzani mkubwa kati ya Wazayuni. 

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO