Tuesday, January 01, 2013

NAM YAZIDI KUIBANA ISRAEL

Jumuiya ya Nchi Zisizofungamana na Siasa za Upande Wowote NAM imeukosoa utawala wa Kizayuni wa Israel kutokana na kuendelea na ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kiyahudi katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu. Jumuiya ya NAM imeukosoa mpango wa hivi karibuni wa Israel wa kutaka kujenga vitongoji vipya vya walowezi wa Kiyahudi na kubainisha kwamba, inalaani vikali mpango huo ambao sio halali. Jumuiya ya Nchi Zisizofungamana na Siasa za Upande Wowote NAM imesisitiza kwamba, hatua ya Israel ya kupora ardhi za Wapalestina ni kinyume kabisa na sheria za kimataifa na kwamba, Tel Aviv inapaswa kusitisha mara moja mwenendo huo haramu wa ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kiyahudi. Jumuiya ya NAM ambayo inaundwa na nchi wanachama 120 imeutaka Umoja wa Mataifa uushinikize utawala wa Kizayuni wa Israel ili usitishe hatua zake pamoja na mashinikizo yake dhidi ya Wapalestina. Inafaa kuashiria hapa kwamba, licha ya kilio na malalamiko ya jamii ya kimataifa dhidi ya ujenzi wa vitongo vya walowezi wa Kiyahudi, lakini utawala ghasibu wa Israel umetia pamba masikioni na kuendeleza ujenzi huo kwa ujeuri sambamba na jinai zake za kila uchao dhidi ya Wapalestina.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO