Thursday, February 28, 2013

WAMAGHARIBI WAPANDIKIZA CHUKI ZA KIDINI SUDAN

Chama tawala nchini Sudan kimeonya kuhusu njama za nchi za Magharibi za kutaka kuzusha vita vya kidini na kikabila nchini humo. Qutbi al Mahdi mmoja wa viongozi wa chama tawala cha Kongresi ya Kitaifa ya Sudan amesema nchi za Magharibi zinataka kuwalazimisha watu wa Sudan wawe Wakristo sambamba na kuibua hitilafu za kikabila nchini humo lengo likuwa ni kuipokonya nchi hiyo utambulisho wake asili.
Al Mahdi amenukuliwa na tovuti ya Muhit akisema kuwa, utawala wa Kizayuni ukishirikiana na wakuu wa nchi za Magharibi wana lengo la kuhakikisha kuwa Sudan inageuka na kuwa nchi kibaraka. Amesema kutokana na kupenya majasusi wengi wa kigeni nchini humo sasa kuna haja ya Sudan kubadilisha mikakati yake ili iweze kukabiliana na tishio lililojitokeza. Al Mahdi ameongeza kuwa nchi za Magharibi zinataka kuidhoofisha Sudan ili kuzuia Uislamu kuenea zaidi barani Afrika. Ikumbukwe kuwa eneo la Sudan Kusini lilijitenga na Sudan mwaka 2011 kufuatia uchochezi wa nchi za Magharibi hasa Marekani na Utawala wa Kizayuni wa Israel. Serikali ya Sudan vile vile inaituhumu Israel kuwa inahusika na kuchochea mapigano ya kikabila katika jimbo la Darfur Magharibi mwa nchi hiyo.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO