Wednesday, March 27, 2013

LARIJANI ASIFU UWEZO JESHI LAKE


Ali Larijani Spika wa Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu ya Iran amesema vikosi vya kijeshi vya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ndio vikosi bora katika kanda hii. Larijani ameyasema hayo leo Jumatano alipokutana na makamanda wa Jeshi la Wanamaji la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika eneo la Konarak, kusini mashariki mwa Iran. Larijani ameongeza kuwa harakati za nchi za Magharibi katika eneo la Ghuba ya Uajemi zinatokana na hofu yao kuhusu jeshi la Iran lenye nguvu na uzoefu.
Larijani ameongeza kuwa kundi la 5+1 linapofanya mazungumzo na Iran hubainisha masuala kinyume na inavyoashiriwa katika vyombo vya habari. Amesema kundi hilo linalojumuisha nchi za China, Russia, Ufaransa, Uingereza, Marekani na Ujurumani wakati zikiwa katika mazungumzo hukiri kuwa tatizo la nchi za Magharibi na Iran si kadhia ya nyuklia bali tatizo ni kuwa hivi sasa Iran inaibuka kama nchi yenye nguvu, yenye kujitegemea na iliyo na vikosi imara vya kijeshi. Larijani amesema Iran ndio nchi pekee katika eneo yenye utawala wa Kiislamu unaotegemea nguvu za wananchi. Ameongeza kuwa hakuna shaka kuwa mwamko wa Kiislamu katika eneo hili umepata ilhamu na mvuto kutoka Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO