Thursday, March 28, 2013

RED CROSS YATUMA UJUMBE KWENDA JELA YA GUANTANAMO


Kamati ya Kimataifa ya shirika la Msalaba Mwekundu (ICRC) imetuma ujumbe katika jela ya Marekani ya Guantanamo Bay huko Cuba wiki moja kabla ya muda uliopangwa, kwa kuhofia kuendelea mgomo wa kula unaofanywa na mahubusu wanaoshikiliwa kwenye jela hiyo.
Msemaji wa ICRC Simon Schorno amesema, makumi ya wawakilishi wa jumuiya hiyo na daktari wameelekea kwenye jela hiyo ya kutisha ya Marekani. Taarifa zinasema kuwa, mgomo wa kula wa wafungwa wa jela ya Guantanamo umeingia siku ya 50, ambapo wafungwa 31 wanagoma kula kwenye jela hiyo. Maafisa wa jela hiyo wanasema kwamba, mahabusu watatu wanaogoma kula wamelazwa hospitali baada ya hali zao kuwa mbaya. Wafungwa wa jela hiyo walianza kugoma kula Februari 6 wakilalamikia uamuzi wa maafisa wa jela hiyo wa kuwanyang'anya baadhi ya vitu vyao binafsi kama barua, cd, picha na nakala za kitabu kitukufu cha Qur'ani.
Jela hiyo ya Marekani ina mahabusu 166 kutoka nchi mbalimbali duniani na watetezi wa haki za binadamu wamekuwa wakikosoa vikali Marekani kutokana na mateso na manyanyaso yanayofanywa dhidi ya wafungwa wa jela hiyo.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO