Tuesday, April 02, 2013

MATEKA WA KIPALESTINA AUWAWA JELA ISRAEL

Atwaullah Abulsabah, waziri wa serikali halali ya Palestina anayeshughulikia masuala ya Wapalestina wanaoshikiliwa katika jela za Israel, ametangaza kuuawa shahidi mateka wa Kipalestina Maysra Abu Hamdiya katika jela za utawala huo wa Kizayuni. Hayo yamejiri baada ya utawala wa Israel kutangaza habari ya kufariki dunia kwa mateka huyo akiwa katika moja ya hospitali za Israel. Kufuatia habari hiyo, Abulsabah amewataka Wapalestina kuanzisha Intifadha ya Tatu na kuongeza kuwa, umewadia muda wa Israel kukosa amani. Aidha Atwaullah Abulsabah aliyekuwa akiongea na waandishi wa habari, ameonya kuhusiana na uwezekano wa kuongezeka idadi ya mashahidi katika mateka wanaoshikiliwa katika jela za kutisha za utawala wa Kizayuni. Waziri huyo wa Palestina, ameitaka Jumuiya ya Nchi za Kiarabu kuchukua hatua za dharura kwa ajili ya kuokoa maisha ya mateka wengine walio hai, sambamba na kukata mahusiano yao na utawala huo wa Kizayuni. Wakati huo huo Msemaji wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS Sami Abu Zuhri amesema Israel itajuta kufuatia kuuawa shahidi Abu Hamdiya.

No comments:

Post a Comment

TUPE MAWAZO YAKO